Jumanne, 1 Aprili 2014

Mvua zasababisha kifo Chunya

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi 



MVUA zinazoendelea kunyesha sehemu mbali mbali hapa nchini zimesababisha madhara katika baadhi ya maeneo ikiwa ni pamoja na kusababisha vifo.
Mvua zilizonyesha Machi 30, Mwaka huu  Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya zilisababisha kifo cha mtoto wa miaka minne baada ya kusombwa na maji ya mto uliojaa wakati akijaribu kuvuka akiwa na dada yake.
Marehemu alifahamika kwa jina la Vailet  Mwansopo(4)  na dada yake aliyenusurika kutokana na maji hayo ni Neva  Mwansopo(6) waliosombwa  na maji ya mto Hasano uliopo kitongoji cha Namalama kijiji cha Mpona Kata ya Totowe Wilayani hapa.
Watoto hao walikutwa na janga hilo walipokuwa wametoka nyumbani kwao Mpona kwenda kitongoji cha Hazolombo kinachotenganishwa na mto huo walikotumwa na Mama yao kwenda kumwita Baba yao mzazi Daimon Mwansopo ambaye anaishi na mke mwingine huko.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa Tukio hilo, ambao ni Noel Mwazembe na Mlawa Mhamali walisema kuwa walisikia sauti ya kuomba msaada kwa mtoto Neva ndipo walipokimbilia eneo hilo na kuambiwa kuwa maji yalipomzidi nguvu aliamua kumwachia mdogo wake naye kufanya juhudi za kujiokoa ndipo walipofanikiwa kumwokoa Neva kisha kuanza kumfuatilia nduguye.
Walisema baada ya kufuatilia waliukuta mwili wa marehemu mita mia mbili kutoka eneo la tukio ukiwa umenasa kwenye mizizi ya miti kando kando ya mto huo ndipo walipouchukua kisha kutoa taarifa kwa Mtendaji wa kijiji cha Malangali Yaledi Mwanguku.
Walisema Mtendaji huyo  alitoa taarifa kituo cha Polisi Galula pamoja na  Daktari ambapo waliufanyia uchunguzi mwili wa marehemu na kuwabidhi ndugu kwa ajili ya mazishi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kutoa wito kwa wazazi kuwa waangalifu na watoto ili kuepusha vifo visivyo vya lazima.
Aliongeza kuwa Mvua zinazonyesha wilayani Chunya zimesababisha madhara makubwa ikiwemo uharibifu wa mazao na kuwataka wananchi kuwa waangarifu kwa kutozurura ovyo kutokana na mito mingi kujaa maji.
Mwisho.

KIHUMBE YAZINDUA KITUO CHA VIJANA MBEYA.

 Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, Dk Samwel Lazalo akikata utepe kuzindua kituo cha Vijana mbeya


 Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, Dk Samwel Lazalo, amelipongeza shirika la Walter Reed Program(WRP) linalomilikiwa na watu wa Marekani lenye makao makuu mkoani Mbeya kwa kufadhili miradi inayowanufaisha wakazi wa jijini hapa.

Meneja wa Kihumbe, Ptolemy Samwel, alisema lengo la kuanzishwa kwa kituo hicho ni kutokana na vijana wa kike na kiume kuathirika zaidi na maambukizi ya Ukimwi na kukosekana sehemu maalumu ya kuwakutanisha na kupewa elimu.













Shirika la Kikundi cha Huduma Majumbani Mkoa wa Mbeya(KIHUMBE) limeanzisha kituo cha Vijana katika Kata ya Forest (Foresti ya zamani) Jijini Mbeya.
Meneja wa Kihumbe, Ptolemy Samwel, alisema lengo la kuanzishwa kwa kituo hicho ni kutokana na vijana wa kike na kiume kuathirika zaidi na maambukizi ya Ukimwi na kukosekana sehemu maalumu ya kuwakutanisha na kupewa elimu.
 Alisema Shirika la Kihumbe limeanzisha kituo maalumu cha vijana baada ya kuona vijana wengi jijini hawana sehemu ya kukutana na kujadili matatizo yao iliona ni muhimu kuwepo kwa kituo cha vijana ambacho pia watatumia kujadili njia mbali mbali za utekelezaji wa mkakati wa kuzuia maambukizi ya VVU/UKIMWI.
Aliongeza kuwa kutokana na ukosefu wa ajira kituo kiliamua kuwawezesha vijana kwa kuwapatia elimu ya ujasiliamali kupitia vikundi vyao vilivyopo katika Kata mbali mbali za jijini Mbeya ili kuwawezesha kujua fursa zilizopo na kuweza kuzitumia ili waweze kujiajiri wenyewe.
Alizitaja shughuli zitakazotolewa katika kituo hicho kuwa ni pamoja na kutoa elimu ya VVU/UKIMWI kwa njia za sinema, Elimu ya matumizi sahihi ya kondomu, magonjwa ya ngono, mtandao wa ngono, ngono mtambaluka na ugawaji wa kondomu.
Aliongeza kuwa shughuli zingine zitakuwa ni kutoa huduma za ushauri nasaha na upimaji wa virusi vya ukimwi kwa hiari, huduma ya daktari, michezo mbali mbali ya ndani ya kituo na nje, elimu ya ujasiliamali pamoja na Msaada wa masomo kwa njia ya mtandao.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, Dk Samwel Lazalo, amelipongeza shirika la Walter Reed Program(WRP) linalomilikiwa na watu wa Marekani lenye makao makuu mkoani Mbeya kwa kufadhili miradi inayowanufaisha wakazi wa jijini hapa.
Pongezi hizo alizitoa alipokuwa akizindua kituo cha vijana kinachomilikiwa na kikundi cha Huduma majumbani Mkoa wa Mbeya(KIHUMBE) kilichojengwa chini ya ufadhili wa Shirika la WRP  kilichopo Forest ya Zamani jijini hapa.
Alisema  msaada wa ujenzi huo utawanufaisha zaidi vijana wengi wa Jiji la Mbeya na wageni watakao tembelea kwa kufundishwa maarifa mbali mbali pamoja na elimu juu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.
Alitoa wito kwa vijana na wamiliki wa kituo hicho kuhakikisha wanatumia kama ilivyokusudiwa ili kuwafurahisha walipa kodi wa Marekani ambao ndiyo waliotoa ufadhili kupitia shirika lao la WRP kwa vijana kutumia kupata maarifa mbali mbali yatakayowasaidia katika maisha.
Mkurugenzi huyo aliongeza kwa kuwataka Viongozi wa Serikali katika ngazi ya kata na Jiji sehemu kilipojengwa kituo hicho kuhakikisha wanaunga mkono jitihada za KIHUMBE na WRP ili kupata malengo yanayotarajiwa kutokana na kituo hicho.

Na Mbeya yetu

Friday, March 28, 2014

MTOTO ABAKWA FAMILIA YAAMBIWA MKAYAMALIZE KINDUGU

MTOTO ALIYEBAKWA AKIWA NA MAMA YAKE 




WAKATI asasi na taasisi mbali mbali zikiwemo TGNP, TAMWA na WRP zikipinga vitendo vya ukatili wa kijinsia, hali hiyo imeonekana kutopewa mwitikio na baadhi ya familia.
Kutopewa kwa kipaumbele na kushindwa kuwachukulia hatua wanaofanya vitendo  hivyo kumetokana na Familia moja jijini Mbeya kutaka kumaliza kifamilia suala la ubakaji lililotokea hivi karibuni.
Tukio hilo lilitokea Machi 13 mwaka huu majira ya saa 11 jioni katika Mtaa wa Mapambano Kata ya Iyela wakati mtoto wa kike alipotumwa dukani na Mama yake Mzazi na kukumbwa na tukio hilo.
Mtuhumiwa wa tukio hilo ambaye ni mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Iyela Jijini Mbeya Patrick Ndelwa(18) anatuhumiwa kumbaka Mwanafunzi wa darasa la nne mwenye umri wa miaka nane(jina limehifadhiwa) shule ya Msingi Mapambano Jijini Mbeya.
Hatua ya kufikia wazazi wa pande zote mbili kutaka kumalizana kifamilia imetokea baada ya Jeshi la Polisi kushindwa kufungua jalada la tukio hilo  tangu  Machi 14, mwaka huu lilipolipotiwa.
Aidha jalada la tukio hilo lilifunguliwa Machi 24 mwaka huu huku Polisi wakitaka yafanyike mazungumzo katika pande hizo mbili na kushindwa kuwachukulia hatua waliotenda makosa kama hayo.
Uchunguzi umebaini kufanyika kikao Machi 26,mwaka huu eneo la Mapambano Iyela kilichowakutanisha pande hizo mbili kwa nia ya kulimaliza nyumbani suala hilo huku upande wa mtuhumiwa ukidai kuwa aliyetenda kosa hilo ni yatima.
Aidha imebainika kuwepo kwa mkakati wa kumhamisha mwathirika wa tukio hilo kumpeleka Jijini Dar es Salaam kwa nia ya kupoteza ushahidi na Jalada kutopelekwa kwa Mwanasheria wa Serikali ili kukwamisha taratibu za kumfikisha mtuhumiwa Mahakamani ili kujibu tuhuma zinazomkabili.
Mama Mzazi wa mwathirika wa tukio hilo,Salome Msigwa alisema aligundua kubakwa kwa mwanae alipoanza kumuogesha Machi 13 mwaka huu majira ya saa kumi na mbili jioni na alipomuuliza alijibiwa kuwa aliyembaka ni Patrick Ndelwa ambapo alimtendea unyama huo katika kichochoro karibu ya nyumba yao.
Alisema baada ya kugundua tatizo la mtoto, alitoa taarifa kituo cha Polisi ambapo mtuhumiwa alikamatwa na mtoto kupelekwa kupimwa Hospitali ya Rufaa na kupewa Matibabu huku akitakiwa kufuatilia vipimo vingine Machi 28.
Baadhi ya wadau wamelalamikia kuongezeka kwa vitendo ya ukatili dhidi ya watoto na kwamba vimekuwa vikiongezeka Jijini Mbeya sehemu kubwa imekuwa ikichangiwa na Dawati la Kijinsia la Jeshi la Polisi kutokana na kugeuka Mahakama kuyamaliza matatizo kwa kupatanisha pande zinazotuhumiana.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya Ahmed Msangi amekiri kupokea tatizo hilo kwamba jeshi lake linafanyia uchunguzi swala hilo likikamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani.
Mwisho.

Na Mbeya yetu

Thursday, March 27, 2014

DAWA HATARINI KUHARIBIKA KUTOKANA NA UTUNZAJI MBOVU MALANGALI CHUNYA

 Muuguzi wa kituo hicho Pilly Ntongolo akionyesha jinsi stoo hiyo ya Madawa ya Binadamu ilivyochanganyika na Saruji



 Muuguzi wa kituo hicho Pilly Ntongolo yeye ndie Daktari , Mtunza Ghala na Mkunga  kazi ipo




Hii ndiyo Zahanati yenyewe

Choo sikunyingi kimeziba ni pango la Mijusi na Nyoka sasa

Mgonjwa akisubiri huduma

Dawa zinazosambazwa na Serikali katika zahanati ya kijiji cha Malangali kata ya Totowe wilaya ya Chunya zipo hatarini kuharibika kutokana na utunzwaji mbovu.

Muuguzi wa kituo hicho Pilly Ntongolo amekiri kuwepo kwa tatizo hilo kwa muda mrefu tangu zahanati hiyo kuzinduliwa kwa mbio za mwenge miaka miwili iliyopita huku uongozi wa kijiji na kata kushindwa kuchukua hatua madhubuti.

Ntongolo amesema kuwa dawa hizo zimekuwa zikitunzwa hovyo kutokana na kutokuwepo kwa shelfu za mbao ambazo zingewezesha  kupangwa kwa utaratibu unaoeleweka,lakini imekuwa tofauti baada ya uongozi wa kijiji kushindwa kununua mbao za kutengenezea shelfu hizo.

Hali imekuwa mbaya zaidi baada ya utaratibu mpya wa kusambaza dawa vijijini kupitia mpango wa shirika la Bohari na usambazaji  dawa[MSD]kwa walengwa kuzambaza dawa katika zahanati hiyo kulundikwa hovyo bila utaratibu hali ambayo ina hatarisha usalama wa dawa hizo.

Uchunguzi umebaini kuwa kituo hicho chenye namba za MSD 105866 kuwa na tatizo pia na tatizo kubwa la kuharibika dari baada ya mchwa na popo kuharibu dari na kusababisha dawa hizo kumwagikiwa na vumbi pia na mikojo ya popo hali inayohatarisha afya za watumiaji wa dawa hizo.

Pia zahanati hiyo inakabiliwa na tatizo la kuwepo maji hali inayolazimu muuguzi huyo kulazimika kuchota maji kutoka kwake wakati wa kutoa huduma ya kuzalisha kwa wajawazito wanaofika kujifungua.

Aidha vyoo vya zahanati hiyo vimeziba kutokana na ukosefu wa maji hali inayolazimu wagojwa kujisaidia vichakani kutokana na kukosekana kwa maji hali inayohatarisha afya kwa wagonjwa.

Changamoto nyingine inayoikabili zahanati hiyo ni pamoja na mazingira machafu ambapo nyasi zimeota hadi katika upenu wa zahanati,ambapo muuguzi hulazimika kuacha huduma kwa wagonjwa ili kupunguza uchafu uliokithiri.

Mtendaji wa kijiji hicho Yaledi Mwanguku hakuwa tayari kumpeleka mwandishi katika zahanati hiyo akidai muuguzi hayupo ,lakini mwandishi alipokwenda alimkuta muuguzi hali inayoonesha kutokuwa tayari kujibia kero hii.

Hivi sasa zahanati hiyo haina Mwenyekiti wa Kamati ya Afya kutokana na Ahmed Ndauka kujiuzuru kutokana na tofauti baina yake na muuguzi ambapo Kamati ya Afya ya wilaya ilifika kutatua mgogoro huo.

NaEzekiel Kamanga 
Mbeya yetu

SEMINA DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA KWA WANAHABARI YAFANYIKA JIJINI MBEYA

Mratibu wa Kupinga Vitendo vya ukatili wa  Kijinsia wa Walter Reed Program, Thorm Chacha wakati wa Semina kwa waandishi wa habari iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Mbeya Peak iliyopo jijini hapa.

Makamu mwenyekiti wa Clabu ya waandishi wa Habari mkoa wa Mbeya Modestus Mkulu akifungua Semina hiyo


Gabriel Mbwile moja kati ya wawezeshaji katika semina hiyo

Baadhi ya waandishi wa habari mkoa wa Mbeya wakiwa katika semina hiyo










Vitendo vya ukatili wa kijinsia ni moja ya sababu iliyochangia ongezeko la maambukizi ya virusi vya Ukimwi katika Mikoa ya Kanda ya Nyanda za juu kusini.
                
Hayo yamebainishwa na Mratibu wa Kupinga Vitendo vya ukatili wa  Kijinsia wa Walter Reed Program, Thorm Chacha wakati wa Semina kwa waandishi wa habari iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Mbeya Peak iliyopo jijini hapa.
Alisema sababu hiyo ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Shirika la Walter Reed Programu kwa Kushirikiana na Shirika la Henry Jackson For Medical Research la Marekani ambao unaonesha ukatili wa kijinsia ndani ya familia na Kaya huchangia maambukizi ya virusi vya Ukimwi.
Chacha  alibainisha kuwa utafiti umeonesha  kuwa tabia za wanaume kukwepa majukumu yao ndiyo kiini cha tatizo ya kuongezeka kwa vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na kuchangia kuongezeka kwa maambukizi mapya.
Alisema vitendo vya ukatili vinavyofanywa na wanaume ni pamoja na kutelekeza familia zao hali ambayo imesababisha watoto kutopata malezi ya wazazi wote na hivyo wanajikuta wakiwa katika mazingira hatarishi pindi ndoa zinapovunjika na familia kusambaratika.
Alisema ipo haja kwa mashirika yanayojishughulisha na kupinga vitendo vya ukatili nchini kuweka nguvu zaidi maeneo ya vijijini,maeneo ambayo wanawake wameachiwa mzigo mkubwa wa kulea familia.
Aliongeza kuwa katika kukabiliana na ongezeko la maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi serikali na wadau pamoja na wananchi kwa ujumla mkoani Mbeya wanapaswa kusimamia ipasavyo sheria zilizopo dhidi ya watu wanaodaiwa kufanya ukatili wa kijinsia.
Alisema ili kuhakikisha ukatili wa kijinsia na maambukizi ya ukimwi yanapungua shirika hilo limeanzisha vituo vya kushughulikia ndani ya Mkoa wa Mbeya ambavyo viko katika Wilaya 6, kata 27 na vijiji 121 pamoja na Jiji la Mbeya.
Mwisho.

Na Mbeya yetu

Tuesday, March 25, 2014

SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI UJUMBE WATOLEWA KWA VIJANA


Meneja wa Kanda ya Nyanda za juu kusini magharibi wa Mamlaka ya hali ya hewa, Ahmed Issa, alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya sekondari Wenda walipotembelea kituo hicho katika kuadhimisha siku ya hali ya hewa duniani.

Wanafunzi wa Shule ya sekondari Wenda wakimsikiliza Meneja wa mamlaka ya hali ya hewa


Baadhia ya waalimu na wadau mbali mbali wa jijini Mbeya walihudhuria 


Baadhi ya watumishi wa Mamlaka ya hali ya hewa nyanda za juu kusini wakiwa makini kumsikiliza meneja wako katika siku hiyo ya hali ya hewa Duniani

Wanafunzi wa shule ya Sekondari Wenda wakipata somo fupi la hali ya hewa













SERIKALI imetakiwa kutoa mitaala ya elimu kuhusu hali ya hewa katika shule za Sekondari nchini ili kukabiliana na ongezeko la joto na mabadiliko ya tabia ya nchi katika karne zijazo.
wito huo ulitolewa  na Meneja wa Kanda ya Nyanda za juu kusini magharibi wa Mamlaka ya hali ya hewa, Ahmed Issa, alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya sekondari Wenda walipotembelea kituo hicho katika kuadhimisha siku ya hali ya hewa duniani.
Alisema kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni mabadiliko ya hali ya hewa na vijana hivyo ni muhimu kwa Serikali kuandaa mitaala ya elimu kuhusiana na hali ya hewa ili kuwafanya vijana waelewe njia mbali mbali za kukabiliana na ongezeko hilo kwa miaka ya baadaye kwa kuwa ndiyo watakaokuwepo.
“ Vijana ndiyo watakaokuwepo na kuishi katika karne zijazo, hivyo ni bora tukajikita katika kuwaelimisha wao kwa serikali kuandaa mitaala ya masomo wakiwa mashuleni namna ya kuendana na mabadiliko yanayotokea” alisema meneja huyo.
Aliongeza kuwa tangu mwaka 1850 kumekuwa na kasi ndogo ya mabadiliko ya hali ya hewa kwa joto kuongezeka duniani lakini kadiri muda unavyoozidi kusonga mbele joto linazidi kuongezeka hadi kufikia asilimia 0.75 hadi asilimia moja na utabiri ukionyesha hali kuwa mbaya zaidi.
Alisema hadi sasa zaidi ya asilimia 60 ya ongezeko la joto duniani husababishwa na hewa mkaa angani ambapo njia kuu ya kukabiliana na hali hiyo ni pamoja na upandaji wa miti ya asili kuendana na eneo husika itakayochangia kunyesha kwa mvua yenye manufaa katika jamii.
Meneja huyo alisema hayo yote yanawezekana kukabiliana nayo ikiwa ni kushirikisha vijana na kuwapa elimu mapema na kuzingatia umuhimu wa ufuatiliaji wa taarifa zinazotolewa na mamlaka ya hali ya hewa na jinsi ya kujihami.
Mwisho.

Na Mbeya yetu
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni